Kura ya hapana yatikisa Bunge Maalumu la Katiba

Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta,  akiwaonyesha wajumbe wa bunge hilo, karatasi za kupigia kura zitakazotumika kupitishia vifungu vya Rasimu ya Katiba,  bungeni,Dodoma jana.
Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, akiwaonyesha wajumbe wa bunge hilo, karatasi za kupigia kura zitakazotumika kupitishia vifungu vya Rasimu ya Katiba, bungeni,Dodoma jana.

Wajumbe wa Bunge la Maalumu la Katiba jana walianza kupiga kura za kuamua ibara za Katiba inayopendekezwa, huku kura za wajumbe kutoka Zanzibar zikiibua wasiwasi wa iwapo theluthi mbili itapatikana au la.

Dalili za kupiga kura za hapana kutoka upande wa Zanzibar zilianza kujionyesha mapema baada ya taarifa za ndani kueleza kuwa zikikosekana 10 kutoka upande huo wa Muungano hakuna katiba.

Hata hivyo, mapema Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta alisema idadi ya kura zinazohitajika kukidhi theluthi mbili kwa upande wa Zanzibar ni 140 na jana jioni waliokuwamo bungeni walikuwa 142.

Mjumbe wa kwanza kufungua pazia kwa kura ya hapana alikuwa ni Adil Mohamed Adil aliyepiga ibara zote 157 kwa sura ya kwanza hadi 10.

Wengine waliopiga kura ya hapana kwa sura zote ni Dk Alley Soud Nasoro na Salma Said.

Waliopiga kura za hapana ni Fatuma Mohamed Hassan na Jamila Abeid Saleh, huku baadhi ya wajumbe wakipiga kura za siri.

Kwa upande wake, Ali Omary Juma, alikubaliana na sura za 2, 4, 5 na 9 lakini akizikataa sura za 1,3,6,7,8 na 10.

Kwa upande wa Tanzania Bara, wajumbe Abia Nyabakari na Dk Ave-Maria Semakafu walipiga kura za ndiyo kwa baadhi ya sura na zingine kuzikataa.

Mjumbe Ali Keissy Mohamed aliushangaza ukumbi kwa kupiga kura ya ndiyo kwa sura zote tofauti na wakati akiwa katika vikao vya kamati ambapo alikataa muundo wa serikali mbili.

Watakaopiga kura kwa faksi

Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta jana alitangaza orodha ya wajumbe 22 wanaotarajiwa kupiga kura kwa njia ya faksi au mtandao wakiwa nje ya Bunge hilo.

Katika orodha hiyo, akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Fredrick Werema, wajumbe tisa wako Saudi Arabia kwa ajili ya Hijja, wawili India kwa matibabu, mmoja yuko masomoni Uholanzi na wengine nje ya Dodoma lakini yuko hapa nchini.

Orodha ya wajumbe

Wajumbe walioko Uarabuni ni Dk Abdalah Kigoda, Mussa Yusuph Kundecha, Hamza Mustapha Njozi, Mohamed Raza, Dk Maua Daftari, Shawana Bukheri Salum, Asha Dodo Mtwangi, Amina Andrew Clement na Riziki Lulida.

Wajumbe walioko India kwa matibabu ni Beatrice Shelukindo na Salum Hassan Turk.

Wajumbe wengine waliko nje ya nchi ni Fredrick Msigala, Waziri wa Afya, Dk Seif Suleiman Rashid, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela na Waziri Mkuu Mstaafu, John Malecela.

Waliopo nchini ni Esther Bulaya, William Lukuvi, Profesa Esther Mwaikambo, Dk Athman Mfutakamba, Saada Salum Mkuya, Dk Henry Nyamubi, Sixtus Mapunda na Dk Natujwa Mvungi.

Mwananchi.

Mahakama ya Kadhi yalitafuna Bunge

Wabunge wakiwa Bungeni mjini Dodoma
Wabunge wakiwa Bungeni mjini Dodoma

Suala la Mahakama ya Kadhi limechafua hali ya hewa bungeni mjini Dodoma baada ya wajumbe Waislamu kutishia kupiga kura ya hapana kama halitaingizwa katika Rasimu inayopendekezwa.

Wakati Waislamu wakishikilia msimamo huo, wajumbe ambao ni Wakristo nao wamejipanga kupiga kura ya hapana endapo Mahakama ya Kadhi itaingizwa katika Katiba inayopendekezwa.

Dalili za mpasuko huo zilianza kujitokeza jana asubuhi baada ya mjumbe mmoja, Jaku Ayub Hashim kuwasha kipaza sauti akitaka kuzungumza akisema ana jambo muhimu.

“Mheshimiwa tangu jana (juzi) ulisema utanipa nafasi ya mwanzo nizungumze,” alisema Jaku, lakini Makamu Mwenyekiti, Samia Suluhu alimtaka aketi chini na suala lake limesikika.

Suluhu akaendelea kuwapa wajumbe wengine kuendelea kuchangia na baadaye alimpa Jaku muda wa dakika saba ili kuwasilisha kile alichotaka kukizungumza ndani ya Bunge hilo.

Jaku alisema walipendekeza kifungu kinachotaka uamuzi unaohusu ndoa, talaka na mirathi iliyoamuliwa kwa misingi ya dini ingizwe kwenye Katiba inayopendekeza lakini hakimo.

“Ni kitu kidogo kabisa tuliomba kiongezwe lakini cha kusikitisha kikundi cha sanaa kimeingizwa. Mimi binafsi yangu sitaunga mkono wala mguu wala sitaipigia kura hii,” alisema Jaku.

Suluhu akamweleza kuwa angalizo lake limechukuliwa, na uongozi wa Bunge pamoja na kamati ya Uandishi wanajitahidi kuingiza kila kitu kinachowezekana, lakini kwa misingi na sheria za nchi.

Baadaye Sheikh Masoud Jongo alipopewa nafasi ya kuchangia, naye alitahadharisha kuwa mambo yaliyopendekezwa na Waislamu yasipoingizwa kama ilivyo kwa sasa, hawatakuwa tayari kwa lolote.

“Msimamo wetu sisi Waislamu kama mambo yetu tuliyoleta katika mapendekezo hayataingizwa, basi yatabomokea hapa na hatutakuwa tayari tena,” alisema Sheikh Jongo, kauli iliyowashtua wajumbe.

Akihitimisha majadiliano hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi, Andrew Chenge alisema kamati yake imefanya kazi kwa uadilifu mkubwa na kwa masilahi ya Watanzania. Akiahirisha Bunge, Suluhu alisema kesho Bunge litaanza kwa kupitia baadhi ya mambo yaliyoibuka katika uhakiki kisha kupitisha azimio la upigaji wa kura. Kura zitapigwa kati ya kesho hadi Oktoba 2.

Baada ya kuahirishwa kwa Bunge, Sheikh mwingine, Hamid Jongo alimwendea Askofu mstaafu Donald Mtetemela na kumkumbatia, kisha kumvuta pembeni na kisha kuteta kwa dakika tano.

Katika viwanja vya Bunge, hali ilikuwa tete kwani kulikuwa na makundi tofauti tofauti ya Wakristo na Waislamu kila moja likijadili na kutafakari suala la Mahakama ya Kadhi kuingizwa kwenye Katiba.

Mjumbe wa kundi la 201 Dk Aley Nassoro alisema kuwa suala la Mahakama ya Kadhi lisipoingizwa katika Katiba inayopendekezwa, atakuwa wa kwanza kuhamasisha wenzake ili wagome kupiga kura.

Dk Nassoro alisema Waislamu wamechoka kudanganywa kwani tangu kipindi cha kampeni za mwaka 2010, waliahidiwa kuwa jambo hilo lingeshughulikiwa mapema lakini watawala wamekuwa kimya.

“Hii Katiba itakuwa ni mbovu kuliko ile ya mwaka 1977 na italeta migongano baada ya miezi sita tu tangu kuzinduliwa. Bora iachwe kwani mambo mengi ya msingi kwa Wazanzibari yameachwa,”alisema.

Akiwa viwanja vya Bunge Askofu Mtetemela alionekana akishauriana na wajumbe mbalimbali na baadaye alisema analaani kauli hizo na kusema kuwa hazilengi kujenga nchi badala yake zinabomoa.

“Kinachotakiwa ni amani, sasa tukianza kutishiana mambo hayatakwenda maana na sisi Wakristo tutataka mambo yetu yaingizwe humo, tunachohitaji ni amani na si vinginevyo,” alisema Mtetemela.

Askofu Mtetemela alisema kikubwa kinachotakiwa kwa wajumbe ni maridhiano na isiwe vitisho kwa kuwa walianza pamoja hivyo wanapaswa kumaliza pamoja.

Aliitaka Kamati ya Uandishi kutoingiza kabisa jambo hilo katika Katiba na akasema hali ikifikia hapo itasababisha mgogoro wa kimasilahi kwa kila mtu kudai haki yake ndani ya Katiba.

Hata hivyo, aliitaka Serikali kutunga sheria za kutambua uamuzi wa Waislamu wa ndoa, mirathi na umiliki wa rasilimali kwa Waislamu ili yakubaliwe kwenye sheria siyo kwenye Katiba.

Mjumbe mwingine wa Bunge hilo, John Cheyo, alitaka Watanzania kuendelea kuheshimu Katiba ambayo imeweka wazi kuwa Serikali haina dini bali wananchi wake ndiyo wenye dini.

“Kwa sababu ukienda njia hiyo hakuna atakayeshinda. Na sisi Wakristo tuseme bila ‘Canon Law’ (Sheria za Kanisa) hakuna hatupigi kura, tutafika wapi? Ndiyo maana tuliyatenganisha haya mambo,”alisema.

Wakati makundi hayo yakiwa na msimamo tofauti, jana katika viwanja hivyo vya Bunge walisikika Waislamu wakihamasishana kwamba kama ikifika kesho hakuna Mahakama ya Kadhi wasusie Bunge.

Suala la Mahakama ya Kadhi, linaonekana kuwapasua kichwa wajumbe wa Kamati ya Uongozi ambayo juzi na jana zilikutana kutafuta njia ya kulinusuru Bunge hilo na mpasuko huo mkubwa.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho, zilieleza kuwa baadhi ya wajumbe walipendekeza kuitishwa kwa Kamati ya Maridhiano ili kutafuta njia bora itakayonusuru Katiba Mpya kukwama kesho.

Mwananchi.

Warioba: Nitaendelea kuitetea Rasimu, sitakimbilia Ukawa

Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Katiba Jaji Joseph Sinde Warioba.
Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Katiba Jaji Joseph Sinde Warioba.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema uamuzi wake wa kuitetea Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na tume aliyoiongoza, pamoja na kauli yake ya juzi ya; ‘Tutakutana mtaani’, havimaanishi kwamba atakihama Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Jaji Warioba amesema jana kwamba baada ya kutoa kauli hiyo katika maadhimisho ya miaka 19 ya Kituo cha Sheria na Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), baadhi ya watu wakiwamo makada wa CCM wanaodhani kuwa atajiunga na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) katika maandamano ya kudai Katiba Mpya iliyotokana na maoni ya wananchi.

Katika kongamano hilo, Jaji Warioba alisema Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba Septemba 24 mwaka huu bungeni mjini Dodoma, imeondoa mambo manne muhimu na mengine mengi yaliyokuwa kiini cha kupata Katiba ya mageuzi.

Akizungumza na gazeti hili Jaji Warioba alisema: “Juzi (jana) niliposema kuwa tutakutana mtaani, nilikuwa namaanisha kwamba tutakutana na Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba katika midahalo, makongamano, semina na katika vyombo vya habari. Sisi tutaendelea kuitetea rasimu tuliyoitoa Desemba mwaka jana. Wao (wajumbe wa Bunge la Katiba), tutakutana nao huko huko ili wawaeleze wananchi sababu za kuondoa maoni yao.”

Jaji Warioba aliyeiongoza Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa miezi 20 ikiratibu na kukusanya maoni ya wananchi na mabaraza ya katiba ngazi mbalimbali, alisema kuwa kamwe hawezi kujiunga na Ukawa unaoundwa na vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF, NLD na DP kwa sababu vyama vya siasa viliuteka mchakato huo na kuuharibu.

“Ieleweke kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba inasimamia katika maoni ya wananchi na haiwezi kuyumba katika hilo. Tutaendelea kusisitiza kuheshimiwa kwa maoni hayo na wale waliyoyabadilisha, lazima wawaeleze wananchi sababu za kufanya hivyo,” alisema.

Aliongeza: “Inashangaza kuona watu wakihusisha kauli yangu ya juzi na kujiunga na Ukawa au vyama vya siasa. Tusubiri tu, ikifika wakati wa kupiga kura ya maoni ili tuone wananchi watakubali rasimu ipi.”

Katika ufafanuzi wake, Jaji Warioba alisema kuwa hata suala la mgombea huru limewekwa masharti mengi yanayoweza kuwa kikwazo kwa mgombea.

“Mgombea huru kawekewa masharti ambayo binafsi naona kama ni ya kumkataa kistaarabu. Suala la muungano nalo pia ni tatizo na bado halijapatiwa ufumbuzi,” alisema.

Mwananchi.

ZLS: Katiba ya wananchi imeporwa na watawala

Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS) Awadh Ali Said
Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS) Awadh Ali Said

Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS), Awadh Ali Said amesema Rasimu ya Katiba inayopendekezwa na Bunge Maalumu la Katiba imepora mamlaka ya wananchi kutokana na kitendo cha kubadilisha vifungu muhimu ikiwamo mfumo wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Akizungumza jana na gazeti hili mjini Zanzibar, Awadh alisema kitendo cha kubadilisha mfumo wa Muungano wa serikali tatu kama ilivyokuwa imependekezwa na rasimu ya awali ya Jaji Joseph Warioba ni kuvunja msingi wa nyumbani na kinakwenda kinyume na maoni ya wananchi.

Alisema kwamba mfumo wa Muungano wa Serikali mbili na marekebisho yake yaliyofanyika umekuwepo katika miaka ya nyuma na katika kipindi cha miaka 50, lakini umeshindwa kuondoa kero za Muungano.

“Bahati mbaya mchakato wa katiba umeporwa kutoka kwa wananchi na kumilikiwa na watawala kinyume na matakwa ya wananchi, hatuwezi kupata katiba bora kwa kuweka masilahi binafsi ya vyama.” alisema Awadh.

Awadh ambaye alikuwa Kamishna wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba alisema kitendo cha kubadilisha vifungu vilivyokuwa vimependekezwa katika Katiba ya awali ni sawa na kuondoa maoni ya wananchi kwa vile rasimu ya Warioba ilitokana na maoni ya wananchi wa pande mbili za Muungano kabla kuwasilishwa bungeni Febuari mwaka huu.

Aidha, alisema kwamba wabunge wa Bunge la Katiba kupitia vyama vya siasa wamezingatia masilahi yao binafsi badala ya masilahi ya Taifa na wananchi wake, ndiyo maana wamefuta vifungu muhimu kama kuwapo kwa ukomo wa kugombea ubunge, kiwango maalumu cha taaluma, wananchi kuwa na mamlaka ya kikatiba ya kumwondoa mbunge asiyewajibika kwa madhumuni ya kuimarisha uwajibikaji na misingi ya utawala bora nchini.

“Jambo la msingi Bunge la Katiba livunjwe, liundwe bunge jipya lisiloshirikisha wabunge wanaotokana na vyama vya siasa ili tupate katiba bora na yenye manufaa kwa wananchi wa pande mbili za Muungano wetu,” alisema Awadh.

Akifafanua, alisema hatua ya wabunge kuingiza mambo ya bahari na ardhi katika orodha ya mambo ya Muungano kutaibua kero nyingine mpya, kwa sababu haiwezekani kuondoa mambo ya mafuta na gesi katika orodha ya mambo ya Muungano wakati rasilimali hizo zinapatikana chini ya ardhi katika mwambao wa bahari.

Hata hivyo, upande wake Mwanasheria Mkuu wa zamani, Hamid Mbwezeleni alisema kwamba rasimu ya mwisho ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano siyo mbaya baada ya kufanyiwa marekebisho mbalimbali na kutaka wabunge wa Bunge la Katiba kupewa nafasi ya kukamilisha majukumu yao.

Alisema kwamba, iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba wakati ikitekeleza majukumu yake hakuna mhimili ambao uliingilia majukumu yake na kushangazwa na kitendo cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo kugeuka msemaji mkuu wa Watanzania.

Mwananchi.

Majambazi wapora milioni 30.6 wajeruhi Polisi, Mfanyabiashara

Sajenti Hija Hassan Hija akipatiwa huduma ya kwanza katika Hospitali ya Mnazi Mmoja mara baada ya kujeruhiwa kwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni mjambazi maeneo ya Mlandege.
Sajenti Hija Hassan Hija akipatiwa huduma ya kwanza katika Hospitali ya Mnazi Mmoja mara baada ya kujeruhiwa kwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni mjambazi maeneo ya Mlandege.

Na Tatu Makame, Laylat Khalfan

WATU wawili akiwamo askari mmoja wamenusurika kifo baada ya kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, waliofanikiwa kupora mfuko wa fedha unaosadikiwa kuwa na zaidi ya shilingi milioni 30.
Tukio hilo, lilitokea jana mchana majira ya 8:30 katika Mtaaa wa Mlandege Mkoa wa Mjini Magharibi, ambapo majambazi hao walimvamia mmoja wa wafanya biashara wa Mchele hapa nchini aliyetambulika kwa jina la Salum Issa Suleiman (50), Mkaazi wa Baghani Mjini Unguja ,, ambaye walimpora mfuko wake wa fedha hizo wakati akiwa njiani kuzipeleka benki.
Mfanyabiashara wakati akiwa njiani alijikuta akizingirwa na mojaya gari ndogo na kuanzakushambuliwa kwa risasi ambazo zilimjeruhi sehemu zake za miguuni na ghafla kuanguka na ndipo majambazi hao walipowezakufanikiwa kumpora fedha hizo.
Wakati tukio hilo likitokea mmoja wa askari  polisi wa Kituo cha Malindi Sajenti Hija Hassan Hija, alijaribu kupambana namabambazi hao, lakini alishindwa kufanikiwa baada na yeye kujeruhiwa sehemu ya mkononi na mguuni kutokana kushambuliwa kwa risasi.

Wakizungumza na gazeti hili, waathirika wa tukio hilo,  Mfanya biashara Salum alisema, wakati alipokuwa akielekea maeneo ya Benki hiyo  ndipo ilipotokea gari ndogo mbele yake na kumnadia mwizi na hapo ndipo walipompiga risasi ya mguu wa kulia na kumnyang’anya fedha hizo na kuondoka nazo .
Kwa upande wake askari Hija alisema, alipofika maeneo hayo ndipo alipomkuta Mfanyabiashara huyo akiwa katika harakati za kujinasua na  hali  na ndipo askari huyo alipokwenda kumuokoa lakini na yeye alishambuliwa na majambazi hao na kufanikiwa kuondoka na kitita hicho cha fedha zamfanyabiashara huyo,,
Hata hivyo,  majeruhi hao bado wanaendelea kupata matibabu katika Hospitali kuu ya Mnazi mmoja na hali zao walieleza kuwa zinaendelea vizuri.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi,  Mkadam Khamis Mkadam, alisema ni kweli tukio hilo limetokea  na aliyeporwa fedha hizo ni  Mfanyabiashara   wa Mchele katika maeneo ya Bandarini ambae alikuwa akielekea katika Benki ya PBZ tawi la Mlandege.
Alisema mfanyabiashara huyo alikuwa na fedha zenye thamani ya shilling milioni 30,6,00,000, ambazo ni mali ya tajiri wake anafahamika  kwa jina la Yussuf Mohamed, ambazo alikuwa anakwenda kuziweka katika Benki hiyo.
Hata hivyo, Kamanda Mkadam, alitoa wito kwa Wananchi wakati wanapokwenda kuweka pesa kuacha kwenda kwa miguu na kuwatumia askari kwani askari wapo kwa ajili yao ili kuimarisha usalama wa raia.

 

Shirika la UNFPA Yakabidhi magari ya Wagonjwa Zanzibar.

Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mh. Rashid Seif  wakati akilijaribu moja ya gari hilo zilizotolewa na UNFPA katika hafla ilizofanyika  Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.
Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mh. Rashid Seif wakati akilijaribu moja ya gari hilo zilizotolewa na UNFPA katika hafla ilizofanyika Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Zanzibar.

Na RAMADHANI ALI /MAELEZO ZANZIBAR

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu (UNFPA) limekabidhi  msaada wa magari manne ya Ambulance  kwa Wizara ya Afya ya Zanzibar ambayo yatatumika katika Hospitali nne.

Mwakilishi wa UNFPA Tanzania  Dkt. Natalia Kanem alimkabidhi Waziri wa Afya Rashid Seif Suleiman magari hayo katika sherehe zilizofanyika   Wizarani Mnazimmoja.

Dkt. Natalia alitaka  magari hayo yatumike kwa uangalifu ili  kufikia malengo ya millennia  ya kupunguza idadi ya vifo vya mama wajawazito na watoto wanaozaliwa hasa katika maeneo ya vijijini.

Alisema moja ya sababu inayopelekea vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga ni tatizo la usafiri ambalo linachangiwa na uwezo mdogo wa baadhi ya familia hasa katika maeneo ya vijijini.

Aliongeza kuwa  msaada huo ni  sehemu ya Mpango maalum wa Shirika la Umoja wa  Mataifa  ulioanza  mwaka 2011 na kumalizika Juni 2015  ambao  huenda ukaendelea hadi mwaka 2016 kusadia  masuala ya Afya na Lishe.

Amesema  mpango huo wa miaka minne  ambao unahusisha maeneo  makuu saba unaendeshwa kwa pamoja na Mashirika manne ya Umoja wa Mataifa  ambayo ni WHO, UNFPA, UNICEF na WFPA.

Mwakilishi huyo wa UNFPA amewapongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. Jakaya Mrisho Kkwete na Rais wa Zanzibar Dkt Ali Muhamed Sheina kwa juhudi kubwa wanazochukua katika kuimarisha huduma za  mama wajawazito na watoto wachanga.

Aliesema UN inathamini juhudi hizo na  juhudi za kuimarisha uchumi hivyo aliahidi  kuwa wataendelea  kuunga mkono kuhakikisha mama wajawazito na watoto wanaozaliwa wanaendelea kuishi katika mazingira yaliyo  salama.

Waziri wa Afya  Rashid Seif Suleiman, alilishukuru Shirika la UNFPA kwa misaada mbali mbali inayotoa kwa Wizara hiyo  na ameahidi kuwa magari hayo yatatumika katika malengo yaliyokusudiwa.

Amekiri kuwa tatizo la usafiri kwa  mama wajawazito Zanzibar limekuwa likiwasumbua wananchi wengi na inafikia wakati akinamama hujifungua wakiwa kwenye gari  wakati wa kupelekwa Hospitali ambazo hazina stara wala hazifai kwa kazi hiyo.

Alieleza matarajio  yake kuwa tatizo hilo kwa sasa litapungua kwa kiasi kikubwa baada ya kupatiwa msaada huo ambao umekuja wakati muwafaka ambapo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaelekeza juhudi zake kuimarisha  huduma za afya mijini na vijijini.

Gari hazo za ambulance ambazo zitapelekwa katika Hospitali ya Kivunge, Mwembeladu, Mkoani na Micheweni zimegharimu shilingi milioni 245,000,000 za kitanzania.

CHANZO: ZANZINEWS.

Sitta apokea meseji za matusi

Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Mh. Samuel Sitta.
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Mh. Samuel Sitta.

Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta amesema anapokea meseji za simu zaidi ya 50 kwa siku za kumtukana na kusisitiza ataendelea kupambana kuhakikisha Katiba inayopendekezwa inapatikana.

Sitta alitoa kauli hiyo bungeni mjini Dodoma jana wakati akielezea kutoridhishwa kwake na kile alichodai ni namna hukumu ya kesi iliyofunguliwa na Saed Kubenea inavyopotoshwa na wanaomchukia.

“Kuna baadhi ya vyombo vya habari wananichukia mimi binafsi. Wasichanganye chuki hizo na mchakato wa Bunge Maalumu,” alisema Sitta na kuongeza;

“Mimi napokea matusi kila siku. Meseji zisizopungua 50 viongozi wa Chadema wameweka namba zangu katika tovuti nitukanwe kila siku hilo mimi niko tayari na mnaniona niko safi tu wala sihangaiki nalo.”

“Lakini sasa Bunge Maalumu ni chombo cha kikatiba,  kiko tofauti na mwenyekiti wake. Huwezi kuliadhibu Bunge Maalumu kwa sababu hupendi sura ya mwenyekiti wake,” alisema.

Sitta alienda mbali zaidi na kusema, “Kwa hiyo wale wanaoendeleza hayo mapambano tuendelee na tutaendelea kupambana, lakini kazi ya Bunge Maalumu itaendelea na ndugu zangu Watanzania mjue tunaandaa Katiba safi na rafiki kwa wananchi na itapatikana.”

Sitta alisema baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo ya kesi ya Kubenea dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), kumekuwa na tafsiri alizosema ni potofu.

Baada ya maelezo hayo alimpa ruksa AG, Jaji Frederick Werema kutoa ufafanuzi.

Jaji Werema alisema Mahakama Kuu, katika kutafsiri kifungu cha 25(1) (2) inakiri kwamba kuna tofauti kati ya kifungu kilichoandikwa Kiswahili na kile kilichoandikwa Kiingereza.

Alisema Mahakama Kuu katika hukumu hiyo imesema mamlaka ya kuandika Katiba Mpya ina maana ni mamlaka ya kuandika na kupitisha katiba inayopendekezwa kwa ajili ya kupelekwa kwa wananchi kwa ajili ya kupigiwa kura ya maoni.

Mwananchi.

Jaji Warioba: Tutakutana mtaani

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Mstaafu Joseph Warioba akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Miaka 19 ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dar es Salaam jana.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Mstaafu Joseph Warioba akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Miaka 19 ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dar es Salaam jana.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba imeondoa mambo manne muhimu yaliyokuwa kiini cha kupata Katiba ya mageuzi.

Akiyataja mambo hayo muhimu ambayo ni maadili ya viongozi wa umma,  madaraka ya wananchi, mgawanyo wa madaraka na muungano. “Tutakutana mtaani. Tume tutaendelea kutetea rasimu yetu na wao wawaeleze wananchi kwa nini wameondoa maoni yao yaliyokuwa katika Rasimu ya Pili ya Katiba,” aliongeza kwa ufafanuzi Jaji Warioba.

Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 19 tangu kuanzishwa kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) Dar es Salaam jana, Jaji Warioba alisema rasimu hiyo inatofautiana kwa kiasi kikubwa na rasimu iliyotolewa na tume hiyo Desemba mwaka jana.

“Sina hakika kama tutapata Katiba Mpya labda Katiba iliyoboreshwa. Rasimu au Katiba itakayopendekezwa na Bunge Maalumu haitapigiwa kura hadi 2016. Sina hakika kama kura hiyo itapigwa kwa kuwa hakuna maridhiano hasa kuhusu muungano,  rasimu hiyo itaanza kupingwa tangu siku ya kutolewa kwake,” alisema.

Aliongeza, “Wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka kesho Katiba Mpya itakuwa agenda, na agenda hiyo inaweza kuigawa nchi. Kuna uwezekano mkubwa kwamba mwaka 2016 badala ya kupiga kura mchakato ukaanza upya.”

Jumatano wiki hii Mwenyekiti wa kamati hiyo, Andrew Chenge aliwasilisha rasimu hiyo bungeni na kueleza kuwa kamati yake imefuta ibara 28 zilizokuwa katika rasimu ya Jaji Warioba na kuacha ibara 47, kuongeza ibara 42 na kurekebisha ibara 186.

Alisema rasimu hiyo ina sura mpya mbili ambazo ni Mamlaka na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na nyingine inayohusu Ardhi, Maliasili na Mazingira ambayo haikuwekwa katika rasimu ya Warioba kwa kuwa si mambo ya muungano.

Rasimu hiyo ilirejesha muundo wa Serikali mbili kama ilivyo sasa na kutupilia mbali muundo wa Serikali tatu uliopendekezwa na Tume ya Jaji Warioba.

Huku akiwa makini, Jaji Warioba ambaye alitumia saa 1:02 kufafanua umuhimu wa mambo manne yaliyoachwa katika rasimu iliyotolewa na Bunge la Katiba, alisema hivi sasa wajumbe wa Bunge la Katiba wana msemo wao kuwa “Warioba ni shida”, kufafanua kuwa watakapomaliza vikao vya Bunge hilo Oktoba 4, mwaka huu na kurejea mtaani walipo wananchi ndiyo watajua nani ni ‘shida’, kati yake na wao.

Akizungumzia kitendo cha Bunge hilo kubadili kanuni ili kuruhusu wajumbe wake kupiga kura za kupitisha rasimu hiyo kwa baruapepe (e-mail) na nukushi (fax) wakiwa nje ya nchi, Jaji Warioba alisema, “Utaratibu huu hauwezi kutuletea Katiba ya maridhiano. Hata mimi nimeanza kukata tamaa.”

Huku akishangiliwa kila mara na mamia ya watu waliohudhuria kongamano hilo, wakiwamo wasomi na baadhi ya waliokuwa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Warioba alisema kila mjumbe wa tume hiyo alikuwa na mawazo yake juu ya Katiba, lakini waliweka kando mawazo yao baada ya kusikia kauli za Watanzania juu ya Katiba wanayoitaka.

Katika maadhimisho hayo,  Jaji Warioba pia alizindua kitabu cha marehemu Dk Sengondo Mvungi kiitwacho ‘Mvungi anapumua Katiba’. Dk Mvungi  aliyekuwa mjumbe wa Tume ya Katiba na mmoja wa waanzilishi wa LHRC, alifariki dunia mwaka jana nchini Afrika Kusini alikopelekwa kutibiwa baada ya kujeruhiwa na majambazi akiwa nyumbani kwake.

Maadili ya Viongozi wa umma

Kuhusu maadili ya viongozi wa umma alisema, “Wananchi walitoa maoni mazito kuhusu maadili ndani ya jamii na maadili ya viongozi. Kutokana na maoni ya wananchi Tume iliimarisha misingi mikuu ya taifa iliyo katika Utangulizi wa Rasimu. Misingi iliyo katika katiba ya sasa ni uhuru, haki, udugu na amani.”

Alisema kutokana na maoni ya wananchi misingi mipya iliongezwa ambayo ni;  utu, usawa, umoja na mshikamano na kwamba wananchi pia walipendekeza tunu za taifa ziwekwe kwenye katiba ambazo ni utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya Taifa (Kiswahili ).

“Bunge Maalumu limeondoa uadilifu, uzalendo, umoja, uwazi, na uwajibikaji kutoka kwenye orodha ya tunu za taifa na kuziweka kwenye misingi ya utawala bora. Kila Mtanzania anatakiwa awe mzalendo, kila Mtanzania anatakiwa kuwa mwadilifu, kila Mtanzania anatakiwa aenzi umoja. Inakuwaje mambo haya yahusu utawala tu?” alihoji.

Alisema tunu za taifa ndiyo msingi wa utamaduni na maadili ya taifa, kwamba mwelekeo wa taifa utategemea jinsi wananchi wanavyoenzi misingi mikuu na tunu.

Aliponda kitendo cha Bunge la Katiba kutoweka miiko ya uongozi kwenye Katiba wakati kila siku viongozi wanalalamika juu ya rushwa na ufisadi, pamoja na fedha za umma kuwekwa kwenye akaunti za benki nje ya nchi.

“Katika bara la Afrika, nchi kama Afrika Kusini, Namibia na Kenya zimeweka misingi ya maadili na miiko katika Katiba. Hapa kwetu sheria tulizonazo haziwezi kupambana na rushwa na ufisadi. Sijui kwa nini Bunge la Katiba wameondoa hili,” alisema.

Madaraka ya Wananchi

Jaji Warioba alipinga kitendo cha Bunge la Katiba kuondoa kipengele cha wananchi kuwa na madaraka ya kumwondoa mbunge wao kama hawaridhishwi na uwakilishi wake bungeni, mbunge kutokuwa waziri ili aweze kuwawakilisha vizuri na ukomo wa mbunge kuwa vipindi vitatu .

“Bunge lina kanuni za kuwawajibisha wabunge na wananchi nao wanapenda kuwa na madaraka hayo. Vyama vya siasa vina madaraka ya kuwaondoa wabunge wao katikati ya kipindi. Wananchi nao wanataka watumie madaraka yao,” alisema.

Mgawanyo wa madaraka

Akizungumzia mgawanyo wa madaraka kati ya mihimili ya Bunge, Serikali na Mahakama, alisema pendekezo lao la kumwondoa rais na mawaziri kutoka kwenye Bunge linakataliwa kwa sababu nchi imezoea mfumo wa kibunge kama ilivyo kwa nchi nyingi za jumuiya ya madola.

“Siyo kweli kwamba mfumo wetu ni wa kibunge. Kwenye mfumo wa kibunge mkuu wa nchi hana madaraka ya utendaji. Madaraka hayo yako mikononi mwa Waziri Mkuu ambaye ni mbunge. Hivyo ndivyo ilivyo kwa Uingereza, India, Canada, Australia, New Zealand,” alisema.

Akitolea mfano mwingiliano huo alisema wakati wa kutunga Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, bunge lilitunga sheria lakini baadaye Rais alifanya mazungumzo na watu nje ya bunge na baadaye bunge likalazimika kubadili uamuzi.

 “Tanzania ina mfumo wa urais ambapo rais ni mkuu wa nchi, mtendaji mkuu na amiri jeshi mkuu. Rais na mawaziri wake kuwa sehemu ya bunge ni kuchanganya mamlaka. Hali hii inafanya Serikali kuingilia mamlaka ya bunge na pia bunge kuingilia mamlaka ya Serikali,” alisema.

Aliongeza, “Nchi nyingi zimebadili Katiba zao ili kutenganisha madaraka ya mihimili. Jirani zetu wa Msumbiji na Kenya wamefanya hivyo. Kenya imefanya hivyo na sababu zao zinafanana kabisa na zile ambazo wananchi wa Tanzania walitoa.”

Muungano

Huku akitaja kero 20 za muungano, 11 za Zanzibar na 10 za Tanzania Bara zilizotajwa na wananchi wakati wa kukusanya maoni, Jaji Warioba alisema, “Ingawa Rasimu ya Bunge Maalumu limerudisha madaraka ya rais kuigawa nchi hiyo peke yake haitoshi. Mambo haya ni magumu kubadilika kwa upande wa Zanzibar.”

Aliongeza kuwa ili kufanya mabadiliko kwenye Katiba ya Zanzibar ni lazima mabadiliko yapitishwe kwa theluthi mbili au zaidi ya Wawakilishi.

Mwananchi.

Vitisho vyaanza Kamati ya Uandishi

Makamo wa pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Balozi Seif Ally Iddi akisoma moja miongoni mwa ujumbe wa vitisho kwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wanaotokea Zanzibar unaosambazwa kupitia mitandao ya kijamii alipokuwa akizungumza na Wandishi wa hababri jana Dodoma.
Makamo wa pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Balozi Seif Ally Iddi akisoma moja miongoni mwa ujumbe wa vitisho kwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wanaotokea Zanzibar unaosambazwa kupitia mitandao ya kijamii alipokuwa akizungumza na Wandishi wa hababri jana Dodoma.

MAKAMU wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, ameitaka jamii kuacha kutumia mitandao ya kijamii kutishia maisha ya Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.

Balozi Iddi aliyasema hayo Mjini Dodoma jana wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya vitisho vilivyotolewa kwa wajumbe wa Bunge hilo wa Kamati ya Uandishi katika mitandao ya kijamii.

Alisema si vizuri kuwatishia wajumbe hao kwani waliteuliwa kwenye kamati hiyo kwa mujibu wa sheria.

“Wajumbe wa kamati hii, wanaitwa wasaliti, sijui kwanini wanaitwa hivyo na sijui msaliti ni nani kati ya waliobaki kuandika katiba au waliotoka nje,” alisema.

Aliongeza kuwa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewahakikishia usalama wa kutosha wajumbe hao ili wasidhurike.

“Vyombo vya dola vipo na vitafanya kazi yake, niwahakikishie kwamba, wajumbe hawataendelea kuwa salama hata watakaporudi Zanzibar,” alisema.

Alisema Serikali ya Zanzibar, imeridhishwa na Rasimu inayopendekezwa na Bunge hilo iliyosomwa juzi bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi, Bw. Andrew Chenge.

“Baadhi ya mambo machache yaliyokuwa na ukakasi upande wa Zanzibar, yamefanyiwa marekebisho katika Katiba inayopendekezwa.

“Katika hoja 17 zilizowasilishwa kwenye Kamati ya Uandishi na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, zote zimeingizwa kwenye Katiba isipokuwa tatu ambazo zinaendelea kufanyiwa kazi,” alisema.

Alitumia fursa hiyo kutoa ufafanuzi wa kujiuzulu kwa Bw. Othman kwenye Kamati hiyo akisema alitakiwa kushiriki kama Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar hivyo kutokuwepo kwake si kikwazo cha kupatikana Katiba

“Waliokuwepo katika kamati hii upande wa Zanzibar, walikuwa wanatosha,” alisema.

Majira.

Mahakama yajivua mipaka ya Bunge

Mahakama haina mamlaka ya kuamua ni kwa kiwango gani cha maboresho au marekebisho ambayo Bunge la Katiba linaweza kuyafanya katika Rasimu ya Katiba.” Mahakama
Mahakama haina mamlaka ya kuamua ni kwa kiwango gani cha maboresho au marekebisho ambayo Bunge la Katiba linaweza kuyafanya katika Rasimu ya Katiba.” Mahakama

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imejivua katika mgogoro wa mamlaka ya Bunge la Katiba kuhusu ni kwa kiwango gani bunge hilo lina  mamlaka ya kufanya  marekebisho au kuboresho Rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Badala yake, mahakama hiyo imesema hayo ni masuala ya kisiasa zaidi kuliko kisheria. Mahakama hiyo ilitoa msimamo huo jana wakati ikitoa amri kuhusiana na kesi ya kuhoji mamlaka ya Bunge la Katiba, chini ya kifungu cha 25(2) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011.

Hata hivyo, haikutoa sababu za amri hiyo na badala yake ilisema kuwa itatoa sababu hizo Oktoba 7. Kesi hiyo ilifunguliwa na mwanahabari, Saed Kubenea dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) kwa niaba ya Serikali.

Katika kesi namba 28 ya mwaka 2014, Kubenea alikuwa anaiomba Mahakama hiyo itoe tafsiri sahihi ya kifungu hicho kuhusu mamlaka ya Bunge na pia, itamke kama lina mamlaka ya kuacha maudhui ya Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni.

Wakati wa usikilizwaji wa kesi hiyo, Wakili wa Kubenea, Peter Kibatala akisaidiana na Mabere Marando walisema kwa mujibu wa kifungu hicho, bunge hilo lina mipaka na halina mamlaka ya kuacha maudhui ya Rasimu hiyo.

Akijibu hoja hizo, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju alidai kuwa bunge hilo lina mamlaka ya kufanya mabadiliko yoyote na kwamba, halifungwi na Rasimu hiyo kwa kuwa ni nyaraka ya kazi tu kwa bunge hilo.

Katika amri yake jana, Mahamaka ilisema imebaini kuna utata na mkinzano wa maana katika kifungu hicho katika lugha ya Kiswahili na lugha ya Kiingereza.

Hivyo, mahakama kupiti jopo la majaji watatu waliosikiliza kesi hiyo, Augustine Mwarija (kiongozi wa jopo), Dk Fauz Twaib na Aloysius Mujulizi, ilitoa tafsiri sahihi ya mamlaka ya Bunge hilo baada ya kusoma Sheria yote ya Mabadiliko ya Katiba

Ilisema licha ya utata huo, mamlaka ya kutengeneza masharti ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inamaanisha mamlaka ya kuandika na kupitisha Katiba inayopendekezwa kwa ajili ya kupigiwa kura na wananchi wa Tanzania.

Pia, ilisema mamlaka hayo yatatekelezwa kwa msingi wa Rasimu ya Katiba baada ya kuwa imewasilishwa mbele ya Bunge la Katiba na mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

“Kwa kufanya hivyo, Bunge la Katiba linaweza kuboresha au kuirekebisha Rasimu ya Katiba,” alisema Jaji Mwarija alipokuwa akisoma amri hiyo.

Aliongeza: “Mamlaka hayo yana mpaka tu kama ilivyokuwa kwa shughuli za Tume ya Mabadiliko ya Katiba, katika misingi ya kitaifa na maadili yaliyotolewa katika kifungu cha 9 (2) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.”

Ilisisitiza kuwa hayo ni masuala zaidi ya kisiasa kuliko ya kisheria, isipokuwa tu bila kukiuka kifungu cha 9 (2).

Kifungu hicho kinasema: “Tume ya Mabadiliko ya Katiba itaongozwa na misingi mikuu ya kitaifa na maadili ya Jamii  na kinataja mambo ambayo ni sharti yahifadhiwe na kudumishwa, ikiwamo Jamhuri ya Muungano.”

Akizungumzia uamuzi huo, Wakili Kibatala alisema wameridhishwa na jinsi Mahakama ilivyoweza kutekeleza jukumu lake kwa wakati na wamefurahi kuwa imeitambua Rasimu ya Katiba tofauti na mdaiwa alivyodai kuwa hiyo ni nyaraka ya kazi tu kwa bunge hilo.

Alisema bado Mahakama haikuweza kukata kiu yake na ya mteja wake.

Mwananchi.

Balozi Seif akanusha taarifa zilizochapishwa na gazeti la Mtanzania

2.Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Waandishi wa Habari wa vyombo m bali mbali nchini hapo katika Ukumbi wa Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mjini Dodoma.
2. Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Waandishi wa Habari wa vyombo m bali mbali nchini hapo katika Ukumbi wa Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mjini Dodoma.

Na Othman Khamis OMPR

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekanusha Habari  iliyochapishwa katika Gazeti litolewalo  kila siku la Mtanzania iliyotolewa siku ya Jumatano ya tarehe 24 Septemba, 2014 likiwa na  Kichwa cha Maneno kisemacho

“SIRI ZAVUJA ZA AG ZANZIBAR KUJIUZULU “.

Kanusho hilo limetolewa na Makamu  wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akitoa ufafanuzi mbele ya waandishi wa Vyombo mbali mbali vya Habari katika Ukumbi wa Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mjini Dodoma.

Balozi Seif  alisema Serikali inakanusha suala la sintofamu lililoandikwa na gazeti hilo ambayo imedai kwamba Viongozi wa juu wa CCM walikutana kwa dharura na kuazimia kufukuzwa kazi kwa Mwanasheria Mkuu wa SMZ  kwa kile walichodai kwamba amekisaliti Chama cha Mapinduzi

Alifahamisha kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali hatakiwi kuwa muumini wa Chama chochote cha siasa na ndio maana hata vikao vya chama hatakiwi kuhudhuria.  Hivyo uteuzi wa Kiongozi huyo anayesimamia masuala ya kisheria hufanywa na Rais wa Zanzibar ambae ndie mwenye maamuzi ya kumuweka na kumuondoa.

Akigusia hoja 17 za Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar alizotaka ziingizwe katika Katiba Balozi Seif alisema suala hilo ni kweli na Mjumbe huyo alitakiwa aziwasilishe katika Kamati jambo ambalo alilitekeleza.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanziar alielezea faraja yake kutokana na masuala hayo kuingizwa katika Rasimu ya Katiba ambapo hadi sasa Hoja 4 kati ya hoja hizo 17 bado zinafanyiwa kazi.

Alieleza kwamba kuchaguliwa kwa Mjumbe katika Kamati na kukataa kuhudhuria kama alivyofanya Mwanasheria Mkuu huyo wa SMZ ni maamuzi yake binafsi kwa vile hakuna ulazima wa mjumbe kuchaguliwa huko ikaonekana kama kifungo ingawa atakuwa na wajibu wa kuendelea kufanya kazi katika kamati hadi mwisho wake.

Balozi Seif alisema kwamba Mh.Othman Masoud alitakiwa ashiriki katika kamati kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa upande wa Zanzibar.

Alisema hata hivyo kutokuwemo kwake katika kamati sio kikwazo cha kupatikana kwa rasima ya katiba, kwa vile waliokuwamo ndani ya kamati kwa upande wa Zanzibar walitosheleza kuiwakilisha Zanzibar kikamilifu.

Akigusia upotoshaji mwengine ulioandikwa na gazeti hilo la Mtanzania juu ya masuala 17 aliyotaka Mwanasheria Mkuu wa SMZ yaingizwe katika Rasimu ya Katiba Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Taarifa hiyo si ya kweli kabisa.

Balozi Seif alisema Mawaziri wa Chama cha Wanachi {CUF } hawamo katika Bunge Maalum la Katiba sasa inakuaje washiriki kuchangia masuala ambayo wao kama sehemu ya { Umoja wa Katiba ya Watanzania } UKAWA hawakubaliani na kuendelea kwa Bunge hilo.

“Wapo baadhi ya waandishi wa Habari hawafahamu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendeshwa katika Mfumo wa Umoja wa Kitaifa ulioundwa na Vyama vya CCM na CUF na kama inavyoeleweka CUF hawamo ndani ya Bunge hilo sasa itakuaje washiriki kuchangia masuala hayo? “ Aliuliza Balozi Seif.

Alifahamisha kwamba suala hilo liliripotiwa sambamba na upotoshaji mwengine wa gazetui hilo la mwanasheria huyo kuwasiliana na Rais wa Zanzibar alisema ni uzushi mtupu usio na maana.

Alisema Mh. Othman Masoud kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati wowote na uwezo wa kuwasiliana na Rais au Makamu wa Pili wa Rais kwa mashauriano ya jambo lolote analoona linafaa.

Balozi Seif alithibitisha wazi kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati anaamua kujiuzulu wadhifa wa Ujumbe wa Kamati ya Uandishi Rais wa Zanzibar Dr. Shein alikuwa nje ya Nchi kwa kiziara rasmi ya Kiserikali.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Serikali ya Mapinduzi pamoja na Chama cha Mapinduzi bado kinawaamini wana Habari wa vyombo vyote, hivyo amewaomba waandhishi kujiepusha na tabia ya kuzusha baadhi ya mambo ambayo hayana ukweli wowote.

Balozi Seif aliwataka Wana Habari wote Nchini kujitahidi kutumia kalamu zao vyema kwa kuwaelimisha wananchi masuala ya ukweli badala ya kuwapotosha kwa kuwalisha mambo ya kubabaisha.

Akijibu baadhi ya maswali ya wana Habari hao Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitegemei kuchukuwa hatua yoyote ya kisheriaadhidi ya Gazeti hilo. Lakini ikauomba Uongozi wa Gazeti hilo kuzingatia maadili ili kuendelea kutoa Habari zenye usahihi.

Wakati mwengine tunaelewa kwamba kalamu za waandishi huwaponyoka wakati wanapoandika Habari zao. Lakini kuponyoka huko kusiwe ndio muendelezo wa uchapishaji wa Habari zisizo na nuchunguzi “. Alisisitiza Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameiasa mitandao ya kijamii kujiepusha na tabia ya kuendeleza vitisho wanavyovielekeza kwa wajumbe wa Kamati za Bunge Maalum la Katiba hasa kutoka Zanzibar kwa visingizio vya kuizamisha Zanzibar.

Balozi Seif alisema kilichofanyika na kuendelea kufanywa na Kamati hizo chini ya Bunge hilo ni kutekeleza jukumu walilokabidhiwa na watanzania na inapaswa kuheshimiwa na kila Mwanadaamu.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwahakikishia wajumbe wa Kamati hizo kwamba Serikali kupitia vyombo vya Dola vitazingatia usalama wao na vitakuwa tayari wakati wowote kumchukulia hatua za kisheria mtu ye yote atakayetishia maisha ya wananchi wakiwemo wajumbe hao.

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohamed Aboud Mohamed aliwaeleza Wanahabari hao wa vyombo mbali mbali Nchini kwamba Katiba ni mchakato ambao masuala yote yanafanyiwa uhakiki wa kina.

Mh. Aboud alifahamisha kwamba suala lolote zito linalohusu mambo ya Muungano haliwezi kutekelezwa bila ya kuhusishwa viongozi na wataalamu wa pande zote mbili.

Waraka wa Warioba kwa Wasira

Jaji Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Joseph Sinde Warioba.
Jaji Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Joseph Sinde Warioba.

Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba ameandika waraka kumjibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira kwa kauli yake kuwa ndiye aliyemkimbiza CCM kwenda upinzani mwaka 1995.

Katika waraka wa maandishi alioutuma kwa gazeti hili, Jaji Warioba alisema maelezo ya Wasira dhidi yake katika mahojiano maalumu na gazeti hili hayakuwa sahihi na hivyo akamtaka ajifunze kusema ukweli kwa kuwa mambo anayosema yanaweza kumrudia baadaye.

Waraka wenyewe

Tarehe 22 Septemba 2014, Gazeti la Mwananchi lilitoa taarifa ya mahojiano kati yake na Mheshimiwa Steven Wasira. Katika mahojiano hayo, Mheshimiwa Wasira alisema mimi ndiye niliyemkimbiza CCM.

Tangu mchakato wa Katiba Mpya kuanza nilikuwa napata taarifa kwamba Mheshimiwa Wasira alikuwa amenifanya mtaji wake katika kutetea msimamo wake. Wakati mmoja kuna kiongozi mwenzake aliniuliza kama nina ugomvi binafsi na Mheshimiwa Wasira kwa sababu kila akipata nafasi kwenye vikao vyao ananishambulia. Wakati wa mabaraza ya Katiba nilipata taarifa za aina hiyo. Nilichofanya ni kuwaarifu viongozi wake wa CCM.

Mengi aliyosema Mheshimiwa Wasira siyo ya kweli. Napenda nitoe ufafanuzi kwa machache yafuatayo:-

Niligombea mara mbili na Mheshimiwa Wasira. Baada ya Uchaguzi wa 1990 ambao nilishinda kwa kura nyingi sana, uchaguzi huo ilitenguliwa kwa sababu nilifanya kampeni kwa kutumia gari la Waziri Mkuu.

Uchaguzi ulirudiwa mwaka 1992. Niliunda timu ya kampeni, Mheshimiwa Wasira akiwa kiongozi. Aliniomba atangulie jimboni kuandaa mazingira. Alipofika huko akaanza kampeni dhidi yangu na kutangaza kwamba anagombea. Wakati huo kura za maoni zilikuwa zinapigwa na wajumbe wa halmashauri kuu ya wilaya. Wajumbe walikuwa kama 600. Nilipata kura 400 na Mheshimiwa Wasira alipata kura chache akiwa mtu wa tatu au nne. Baada ya matokeo akatangaza anajitoa kwenye mchakato na jina lake lisipelekwe NEC. Alikataliwa kwa sababu kufuatana na kanuni, muda wa mtu kujitoa ulikuwa umepita.

Mwaka 1995, kura za maoni zilikuwa zinapigwa kwenye kata. Tulianza na Kata ya Sarama ambayo iko upande wa mashariki, siku ya tatu tulifika Nyamuswa ambacho ndicho kijiji ninachotoka. Nyamuswa ilikuwa kituo cha tano kati ya vituo 12.

Baada ya hapo tulielekea magharibi ya jimbo anakotoka Mheshimiwa Wasira. Baada ya kura kupigwa katika Kata ya Guta, Mheshimiwa Wasira alijitoa kwa sababu aliona hawezi kunishinda hata kama angepata kura zote za kata mbili zilizobaki. Siyo kweli kwamba Nyamuswa ilikuwa ya mwisho kupiga kura na siyo kweli wananchi wa kata nzima walipiga kura. Kumbukumbu zote zinaweza kupatikana wilayani na makao makuu ya CCM.

Mheshimiwa Wasira anasema kwamba nilikuwa Jaji na kesi iliyopelekwa mahakamani ni kama kesi ya tumbili kupelekwa kwa nyani, kwa maana kwamba majaji walinipendelea. Kumbukumbu za kesi hiyo zipo. Wakati huo sikuwa jaji. Isitoshe huko nyuma uchaguzi nilioshinda 1992 ulitenguliwa. Kwa nini wakati huo sikupendelewa? Kumbukumbu za kesi zinaeleza kwa nini Mheshimiwa Wasira alifungiwa kugombea kwa kipindi.

Mheshimiwa Wasira ni kiongozi wa Taifa kwa kipindi kirefu. Ni mbunge wangu na namtambua hivyo. Tunaweza kuwa na mtazamo tofauti katika baadhi ya mambo lakini hiyo si sababu ya kusema mambo yasiyo ya kweli kwa nia ya kujijenga kisiasa.

Yeye ni Mjumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM. Yeye ni Waziri mwandamizi. Yeye anafikiria kugombea urais. Ni vizuri basi akajifunza kusema kweli (ambayo ni ahadi mojawapo ya WanaCCM). Akumbuke anayosema yanaweza kumrudia mbele ya safari.

J.S. Warioba

24-09-2014

MWANANCHI.

Katiba Mpya: Ni mchezo wa namba

Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalum la Katiba Andrew Chenge.
Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalum la Katiba Andrew Chenge.

Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba jana ilikabidhi bungeni Rasimu ya Katiba inayopendekezwa ikiwa na ibara 289 kulinganisha na 271 za Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba.

Rasimu hiyo pia ina sura mpya mbili ambazo ni Mamlaka na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na nyingine inayohusu Ardhi, Maliasili na Mazingira.

Akiwasilisha rasimu hiyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Andrew Chenge aliliambia Bunge kuwa Ibara 233 za rasimu hiyo zinatokana na Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Chenge, ambaye aliwahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), alisema ibara 47 za Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba zimebaki kama zilivyokuwa, 186 zimefanyiwa marekebisho, 28 zimefutwa na 41 ni mpya.

Rasimu hiyo ya Katiba inayopendekezwa imefuta kabisa muundo wa Muungano wa shirikisho ambao ungezaa muundo wa serikali tatu na badala yake imerudisha muundo wa sasa wa serikali mbili.

Chenge alisema kamati za Bunge hilo pamoja na wajumbe walio wengi, waliona kuingiza muundo wa shirikisho ilikuwa ni kukiuka makubaliano ya Muungano yaliyofikiwa mwaka 1964.

Kwa kurejesha muundo wa serikali mbili uliokuwa ukipigiwa chapuo na CCM, Rasimu hiyo imependekeza kuwapo kwa makamu watatu wa rais.

Chenge alisema uongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania utakuwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mgombea mwenza atakayekuwa makamu wa kwanza wa rais.

Chini ya muundo huo, Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), atakuwa makamu wa pili wa rais ilhali Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atakuwa makamu wa tatu wa rais.

Chenge alisema mapendekezo hayo yamezingatia ukweli kuwa kuwapo kwa mgombea mwenza anayekuwa makamu wa kwanza wa rais, kutafanya rais na makamu wake kutoka chama kimoja.

Rasimu hiyo inayopendekezwa, imepunguza Tunu za Taifa kutoka saba zilizokuwamo kwenye Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba hadi nne huku mambo ya muungano yakiongezwa kutoka saba hadi 14.

Katika Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Tunu za Taifa zilikuwa ni utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi, uwajibikaji na lugha ya Taifa; sasa zimebaki Lugha ya Kiswahili, Muungano, utu na undugu na amani na utulivu. Tunu tatu ambazo ni uzalendo, uadilifu na umoja zimeondolewa.

Mambo ya Muungano

Katika Rasimu ya Tume, mambo ya Muungano yaliyoorodheshwa ni Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ulinzi na usalama.

Mambo mengine yalikuwa ni uraia na uhamiaji, sarafu na benki kuu, mambo ya nje, usajili wa vyama vya siasa, ushuru wa bidhaa na mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na mambo ya Muungano.

Rasimu inayopendekezwa imetaja mambo ya muungano kuwa ni Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ulinzi na usalama, usafiri wa anga, uraia, uhamiaji, polisi, sarafu na benki kuu na kodi ya mapato inayolipwa na watu binafsi na mashirika, ushuru wa forodha na bidhaa zinazotengenezwa Tanzania na kusimamiwa na idara ya forodha.

Mengine ni mambo ya nje, usajili wa vyama vya siasa, Mahakama ya Juu na Mahakama ya Rufani, elimu ya juu, Baraza la Taifa la Mitihani, Utabiri wa Hali ya Hewa na utumishi Serikali ya Jamhuri.

Mambo mengine ambayo yalikuwa katika Rasimu ya Warioba yaliyowekwa kando ni pendekezo la wabunge kutokuwa mawaziri ikipendekezwa utaratibu wa sasa wa wabunge kuwa mawaziri uendelee kutumika.

Chenge alisema Rasimu ya Katiba inayopendekezwa, imeweka ukomo wa mawaziri kuwa wasizidi 30 wakati naibu mawaziri watateuliwa kulingana na mahitaji mahsusi. Tume ya Warioba ilipendekeza mawaziri wasiozidi 15.

Rasimu hiyo inayopendekezwa imefumua muundo wa Bunge uliopendekezwa na Rasimu ya Warioba kuwa wawe 75 wa kuchaguliwa majimboni na watano kutoka kundi la watu wenye ulemavu, badala yake imesema muundo wa sasa uendelee ukiwa na wabunge 360 kwa sharti la kuwapo uwiano sawa kati ya wanawake na wanaume.

Rasimu hiyo imetupilia mbali pendekezo la mtu anayetaka kugombea ubunge awe na elimu isiyopungua kidato cha nne na kurudisha kuwa ajue tu kusoma na kuandika Kiswahili au Kiingereza.

“Haki ya wananchi kumwajibisha mbunge kabla ya miaka mitano imeondolewa kutokana na mapendekezo ya kamati na wajumbe na watafanya hivyo baada ya miaka mitano,” alisema.

Rasimu hiyo imembana mgombea binafsi wa ubunge kwamba atakoma kuwa mbunge pale tu itakapotokea amejiunga na chama chochote cha siasa nchini.

Pendekezo la Warioba la kutaka Spika wa Bunge na Naibu wake wasitokane na wabunge wa Bunge la Jamhuri au kuwa viongozi wa juu wa vyama, nalo limewekwa kando na badala yake spika kupendekezwa achaguliwe miongoni mwa wabunge au kutoka kwa Watanzania wenye sifa ambao watajitokeza kuomba nafasi hiyo kama ilivyo sasa.

Hata hivyo, Chenge alisema wamependekeza Naibu Spika ni lazima atoke miongoni mwa wabunge.

Mgombea binafsi

Chenge alisema pamoja na kwamba mgombea huru wa nafasi ya urais ni haki ya kikatiba, lakini kamati yake imelazimika kuchukua tahadhari na kuweka masharti juu ya mgombea huyo.

Masharti hayo ni pamoja na kuweka kipengele katika Katiba kinacholitaka Bunge kutunga sheria itakayoweka masharti ya mgombea huru ikiwamo idadi ya watu watakaohitajika kumdhamini.

Pia sheria hiyo itaweka sharti la lazima linalomzuia kujiunga na chama chochote cha siasa, kuainisha vyanzo vya mapato vya kugharimia kampeni zake na kuweka wazi ilani yake ya uchaguzi.

Masuala ya kuingizwa kwa Mahakama ya Kadhi na kuruhusiwa kwa uraia wa nchi mbili ambayo yaliwagawa wajumbe wa Bunge hilo katika makundi mawili nayo hayakuingizwa katika rasimu hiyo.

Kuhusu Mahakama ya Kadhi, Chenge alisema kamati yake imezingatia mijadala ya wajumbe, taarifa za kamati za Bunge hilo na Katiba za nchi mbalimbali katika kufikia uamuzi huo.

Alisema katiba inayotungwa inahusu Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani na Mahakama ya Juu hivyo masuala ya Mahakama ya Kadhi yanaweza kusimamiwa na sheria inayohusu mahakimu.

Kuhusu suala la uraia pacha, Chenge alisema waliozaliwa Tanzania lakini wakapoteza uraia na kuamua baadaye kurudi nchini, watarejeshewa uraia wao baada ya kuukana uraia wa nje. Alisema Watanzania wanaoishi nje ya nchi wakiwa na uraia wa nchi hizo, watakapokuja nchini hawatakuwa na uraia wa nchi mbili, badala yake watapewa hadhi maalumu.

Baada ya kukamilika kwa uwasilishaji huo, Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta alitoa fursa kwa wajumbe wa Bunge hilo kuipitia Rasimu jioni na leo watakutana kwenye kamati zao 12 kwa lengo la kuhakiki ni kwa kiasi gani waliyoyapendekeza wakiwa ndani ya kamati na kwenye mijadala yamezingatiwa.

Kesho wajumbe wote watakutana katika Bunge zima kwa lengo la kuhakiki kwa pamoja kuhusu yale yatakayoletwa na sekretarieti kutoka kwenye kamati za Bunge hilo. Septemba 28, wajumbe hao watakutana tena kwenye kamati kwa lengo la kupewa maelekezo ya namna ya kukaa ndani ya ukumbi na pia namna watakavyopiga kura siku inayofuata.

Sitta alisema upigaji wa kura utaanza Septemba 29 hadi Oktoba 2 na baada ya hapo itajulikana kama rasimu hiyo imepitishwa kwa wingi wa kura wa theluthi mbili kwa pande zote za Muungano au la.

Mwananchi.