Masheikh wana wajibu wa kuisaidia jamii katika kukuza elimu

Makamo wa pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idi kwa niaba ya Rais wa Zanzibar akiufungua  Msikiti wa Kijiji cha Kajengwa utakaotoa huduma za ibada za sala na madrasa kwa waumini wa Kijiji hicho.
Makamo wa pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idi kwa niaba ya Rais wa Zanzibar akiufungua Msikiti wa Kijiji cha Kajengwa utakaotoa huduma za ibada za sala na madrasa kwa waumini wa Kijiji hicho.

Na Othman Khamis Ame – OMPR

Wanazuoni, Masheikh na wazee wote nchini wana wajibu mkubwa wa kuisaidia Serikali Kuu katika jitihada zake za kukuza elimu, kujenga jamii iliyo bora, kulinda amani pamoja na kukataza maovu vikiwemo vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji wa kijinsia.

Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al – hajj Dr. Ali Mohamed Shein wakati akiufunguwa msikiti wa Kijiji cha Tasani  Makunduchi unaokadiriwa kusaliwa na waumini wapatao 200 kwa wakati mmoja wa sala.

Dr. Shein ambae Hotuba yake ilisomwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema katika msaada huo Masheikh wana fursa nzuri ya kuzungumza na waumini wao hasa kupitia hotuba za sala za ijumaa ili kujenga jamii iliyo bora.

Alisema Dini imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa zaidi kwenye suala zima la kukuza maadili mema , malezi ya watoto sambamba na kuendeleza hali ya kuishi kwa upendo miongoni mwa jamii  yote.

Rais wa Zanzibar alieleza kwamba Serikali imedhamiria kutilia mkazo mfumo wa Utawala bora unaozingatia utii wa sheria na kuendeleza mikakati katika kuimarisha uwajibikaji kwa kupiga vita ubadhirifu wa mali za umma.

Alifahamisha kwamba uimarishwaji wa mafunzo ya dini katika misikiti na hata madrasa una mchango mkubwa katika kuisaidia Serikali kuimarisha lengo lake hilo la usimamizi wa Utawala bora pamoja na utekelezaji wa mipango ya maendeleo.

Al Hajj Dr. Ali Mohamed Shein amewapongeza Waumini na Wananachi wa Makunduchi kwa jitihada zao walizochukuwa na hatimae kufanikiwa kupata nyumba mpya ya Ibada.

Alisema Jamii imekuwa  ikushuhudia ongezeko kubwa la ujenzi wa misikiti mikubwa yenye nyenzo za kisasa katika pembe zote za Visiwa vya Unguja na Pemba neema ambayo Mwenyezi Muungu anaendelea kuishusha ndani ya Nchi hii.

Alieleza kwamba ujenzi wa Misikiti mipya ni ishara ya kuendelea kwa imani na mapenzi baina ya waislamu pamoja na kuongezeka kwa nguvu za kiuchumi miongoni mwa wananchi.

Dr. Shein aliikumbusha jamii kujitokeza zaidi katika kuwekeza katika mambo ya kheri kama hili la ujenzi wa misikiti ili kujitengenezea maisha bora ya baadaye na kuachana haya ya duniani ambayo ni ya mpito.

“ Na simamisheni sala na mtoe zaka na mkatieni Mwenyezi Muungu sehemu njema { katika mali yeni iwe ndio zaka na sadaka } na kheir yoyote mnayoitanguliza kwa ajili ya nafsi yenumtaikuta kwa mwenyezi mungu imekuwa bora zaidi na ina thawabu kubwa sana “. Dr. Shein aliikariri suratul Muzzammil aya ya 20.

Alisema ni vyema kwa waliojaaliwa uwezo kuangalia maeneo wanayoishi namna bora ya kutoa sadaka inayoendelea katika kupitia usambazaji wa huduma zinazohitajika na jamii iliyowazunguuka.

Alieleza kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikitekeleza dhamira ya kuhakikisha kuwa wananchi wake wanapata huduma muhimu katika maeneo wanayoishi.

Hata hivyo alisema zipo sababu tofauti zinazochangia kwa kiasi kikubwa baadhi ya wananchi kuendelea kukosa huduma hizo muhimu kwa maendeleo yao ya kijamii ya kila siku.

Aliwapongeza waislamu wote waliochangia pamoja na kushiriki kwenye ujenzi wa msikiti huo juhudi ambazo lazima ziambatane na kuendelea kuutunza  msikiti huo ili uendelee kubakia katika haiba yake ya kupendeza.

Katika kuunga mkono juhudi za waumini hao Balozi Seif  Ali Iddi Binafsi aliahidi kusaidia pampu ya kusukumia maji katika msikiti huo mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa mnara wa tangi la maji.

Mapema asubuhi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kwa Niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alilifungua jengo la Madrasatul Shafiat liliopo katika Kijiji cha Kajengwa Makunduchi.

Akizungumza na waumini hao Dr. Shein alisema ufunguzi wa madrasa hiyo ni kielelezo cha jitihada za wananchi wa kajengwa kwa kushirikiana na viongozi wao katika kutilia maanani haja ya kuwapatia elimu ya dini watoto wao jambo ambalo limefaradhishwa na mwenyezi mungu.

Alisema elimu nizawadi na urithi bora kwa watoto ambao huwajenga kuwa na ucha mungu, kujua utu, kuheshimu haki za watu wenye  imani za dini nyengine sambamba na kumtukuza mola anayeteremsha neema kwa viumbe wote.

Alitoa wito kwa uongozi wa Madrasatul Shafiat kufanya juhudi za makusudi kuisajili Madrasa hiyo ili ifuate taratibu zilizopo pamoja na kutambulika rasmi kiserikali.

Alisema Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kupitia kitengo kinachosimamia elimu ya maandalizina madrasa huzisajili madrasa ili kuzitambua , kusimaia taaluma inayotolewa , kuzipatia misaada ya kitaaluma vikiwemo pia vifaa.

Katika juhudi za kuunga mkono waumini hao wa Kajengwa Makunduchi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa niaba ya Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohd Shein aliahidi kuchangia mafeni yote ya Madrasat Shafiiya, Meza ya Mwalimu, pamoja na Makabati ya Vitabu vya Madrasa hiyo.

Akisoma risala ya walimu na Wanafunzi hao wa Madrasat Shafiiya Mwalimu Abou Simai Mussa alisema madrasa hiyo yenye wanafunzi karibu 150 inatoa mafunzo ya elimu ya Dini na Dunia.

Mwalimu Abou alisema madrasa hiyo hivi sasa imekuwa chem chem. Kubwa ya utoaji wa walimu na masheikh mbao wamekuwa wakitoa mafunzo ya kuongoza ibada katika misikiti mbali mbali ya Jimbo la Makunduchi.

Alimpongeza Mwakilishi wa Jimbo la Makunduchi kwa jitihada zake za kuchangia ujenzi wa msikiti huo zilizofikia zaidi ya asilimia 99% ukigharimu zaidi ya shilingi Milioni 21.3.

Akitoa shukrani kwa niaba ya wananchi na waumini hao wa Jimbo la Makunduchi Mwakilishi wa Jimbo Hilo Al Hajj Haroun Ali Suleiman alisema Uongozi wa Jimbo hilo utaendelea kushirikiana na wananchi hao katika kuhakikisha kwamba kero zinazowakabili zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Al – Haroun alisema tatizo la huduma za maji safi na salama ambalo limekuwa kero kubwa kwa wananchi hao hasa katika eneo la ibada la Msikiti atalishughulikia kwa kushirikiana na viongozi wenzake wa jimbo hilo.

Mapema Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Ngwali aliwakumbusha waumini hao kwamba Madrasa lazima zitumiwe kwa juhudi zote katika kujenga hatma njema  ya dunia na sfari ya milele.

DUNI: Mahujaji hawakuipigia kura katiba inayopendekezwa

Wanachama wa Chama cha Wananchi CUF wakimsikiliza Makamo Mwenyekiti wa Chama hicho , Mh, Juma Duni Haji (hayupo pichani) katika Mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Amani kwa mabata.
Wanachama wa Chama cha Wananchi CUF wakimsikiliza Makamo Mwenyekiti wa Chama hicho , Mh, Juma Duni Haji (hayupo pichani) katika Mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Amani kwa mabata.

Na Nassor Khamis.
Suala la wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba waliokuwa kwenye ibada ya Hijja katika miji ya Makka na Madina chini Saudi Arabia, kupigia kura rasimu ya katiba inayopendekezwa na Bunge hilo sikweli.

Hayo yalielezwa na Makamo mwenyekiti wa Chama cha Wananchi CUF taifa Mh, Juma Duni Haji wakati akizungumza na wanachama wa chama hicho katika viwanja vya Amani kwa mabata wilaya ya Magharibi Unguja.

Mh, Duni ambaye pia ni Waziri wa Miundo mbinu na Mawasiliano wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar alisema, kulingana na hali ilivyokuwa katika ibada ya hijja ni vigumu kwa wajumbe hao kupiga kura kwa njia yoyote kutokana na muda wote kuwa katika ibada.

“Suala la kupigwa kura kwa njia ya mtandao ni uongo kwani hakuna hata mtu mmoja aliyepiga kura kutokana na muda wote kuwa katika ibada” alisema Mh, Duni

“Mimi nilikuweko wakati tupo katika mabanda yetu mahujaji nilimuuliza mmoja wa wajumbe vipi ndio utapigia kura katiba hapa” aliongezaMh. Duni.

Pia alisema kuwa licha ya mahujaji hao kushindwa kupiga kura kwa njia ya mtandao, hakuna afisa yoyote aliyeweza kuendesha zoezi la upigaji kura kutokana na kutokuruhusiwa kuingia kwa mtu yoyote asiyekuwa mwenye kufanya ibada hiyo ya hijja.

Aidha amesema kuwa kutoka na mahujaji hao kutokupiga kura na wengine waliyoikata hadharani theluthi mbili ya wazanzibari ya kupitisha katiba inayo pendekezwa haikutimia.

Akizungumzia Katiba inayopendekezwa alisema, katiba hiyo haina maslahi kwa Zanzibar kwani Katiba inayopendekezwa inafuta utambulisho wa Zanzibar pamoja na kuinyima Zanzibar mamlaka yake ya kujiendesha wenyewe.

Alisema kuwa baadhi ya vipengele vinavyoonyesha kuipa mamlaka Zanzibar ni sawa na kupewa kitu kwa mlango wa mbele na kisha kunyang’anywa kwa mlango wa nyuma kwani vipengele hivyo vipo chini ya mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Vipengele hivyo amevitaja kuwa ni pamoja na Zanzibar kujenga mashirikiano na mashirika ya kimataifa pamoja na uwezo wa kukopa fedha kutoka taasisi mbali mbali za kifedha hadi ipate udhamini kutoka kwa Serikali ya Muungano.

“Eti wanasema sasa Zanzibar inaweza kukopa pamoja na kujiunga na mashirika ya kimataifa baada yakupata udhamini ikiwa huo udhamini haukutolewa pamepatikana kitu hapo?” alihoji Mh, Duni.

Pia alisema kuwa kutokana katiba mpya inayopendekezwa kubainisha kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atachaguliwa kwa kupata zaidi ya asilimia hamsini ya kura zote ni vigumu kwa Mzanzibari yoyote kushika wadhifa huo kutokana na idadi kubwa ya wapiga kura walioko Tanzania Bara.

Alisema kuwa ili kupata uhalali wa Rais wa Muungano, Katiba inayopendekezwa iweke kifungu kinacho onesha kiwango maalum cha kura kutoka kwa wapiga kura wa pande zote za Muungano.

Mh. Duni pia alizungumzia vitendo vya unyanyasaji na udhalilishaji unaofanywa na jeshi la polisi kwa watuhumiwa makosa ya ugaidi huku viongozi wa serikali wakikaa kimya, ni kushindwa kusimamia haki za wananchi wanaowaongoza.

Akitolea mfano wa vitendo vya udhalilishaji kwa watuhumiwa wa makosa mbalimbali yaliyowahi kufanyika huko nyuma askari waliofanya vitendo hivyo walichukuliwa hatua za kisheria ikiwamo kufukuzwa kazi.

Amesema kuwa wakati wa uongozi wa awamu ya kwanza wa Jamhuri Muungano wa Tanzani vitendo vya udhalilishaji wa watuhumiwa waliokuwa mahabusu jijini Mwanza Mwalimu Nyerere aliwawajibisha maafisa wa jeshi la polisi kwa kuwafukuza kazi huku aliyekuwa Waziri wa Mambo ya ndani wakati huo Mzee Ali Hassan Mwinyi kulazimika kujiuzulu wadhifa wake.

“leo wanakuja raia mahakamani wanaonesha suruali zinavyovuja chini kutokana na vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa na Polisi wewe husemi kitu Rais gani wewe” alisema Mh. Duni.

Aidha mh, Duni ametaka sheria zilizotungwa zifuatwe kama inavyostahiki pamoja na kuheshimiwa na watu wote.

Akizungumza katika mkutano huo Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Mh, Nassor Ahmed Mazruy alisema kifungu cha thalathini na nne cha sheria ya mabadiliko ya katiba inayosema kuwa katiba inayopendekezwa itapitishwa kwa zaidi ya asilimia hamsini ya kila upande kimelenga kuchakachua kura za maoni ya kupitishwa kwa katiba hiyo.

Alisema kuwa kifungu hicho pia kinawataka Wazanzibari walioko Tanzania Bara kupiga kura upande wa Zanzibar jambo ambalo haliingia akilini na ina lengo la kuvuruga idadi ya wazanzibari ili waweze kupitisha katiba hiyo.

Aidha alisema kuwa chama cha CUF pamoja na vyama vyengine vya upinzani vinavyounda umoja wa katiba ya wananchi UKAWA kwa pamoja wamesaini mkataba wenye lengp la kushirikaiana katika chaguzi mbalimbali ukiwemo uchaguzi wa serikali za mitaa pamoja na uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 kwa lengo la kuindoa CCM madarakani.

Mapema Mjumbe wa Baraza kuu la Uongozi la CUF Taifa ambae pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Ole Mh, Hamad Massoud Hamad amewataka wanachama wa chama hicho kujiweka tayari kwa uchaguzi mkuu ujao kwa lengo la kuiondoa CCM madarakani.

Amesema kuwa uchaguzi unaofuata chama cha CUF hakitofanya makosa kama chaguzi zilizopita kwa kukubali matokeo yasiyo halali yanayo tangazwa na tume ya uchaguzi Zanzibar kwa kutoa ushindi usiostahiki kwa CCM.

“Uchaguzi wa safari hii CUF haifanyi makosa kama yaliyopita viongozi wa juu tayari wameshajiandaa na nyinyi wananchi jiandaeni tuhakikishe tunaing’oa madarakani CCM ifikapo mwakani” alisema Mh, Hamad huku akishangiriwa na wanachama waliohudhuria mkutano huo.