NIWAPE ZAWADI GANI WAZAZI BABA NA MAMA
Nasomeka Mtandaoni, kuomba zenu hekima
Swali hili ni makini, laniumiza mtima
Naitafuta yakini, nisijefanya hujuma
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Mlipo maburuhani, mliyepewa karama
Nawaomba ihsani, nisije kwenda mrama
Niipate ahueni, moyo upate tuama
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Wazazi ndio kiini, fika niliposimama
Miezi tisa tumboni, alipata tabu mama
Baba yupo mashakani, mke kuvuka salama
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Wazo lapita kichwani, niwapeleke Dodoma
Wafike kule Bungeni, wabunge kuwatazama
Wajifunze kitu gani, majibu yamenigoma
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Ufisadi “namba wani”, wafanye tuso watuma
Hadi miaka sitini, mafao kuja yachuma
Nani atatuauni, katika hii hujuma
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Niwapeleke mbugani, wanyama kuwatazama
Twiga farasi wa kusini, wanasafirishwa wima
Waziri madarakani, avuna asicholima
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Ulaya na Marekani, wafike baba na mama
Niwapandishe ndegeni, wakamuone Obama
Nimegutuka bongoni, wazo hilo sio jema
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Kuwapeleka ni shani, iliyojaa adhama
Kule Hija ibadani, ni Makkati Mukarama
Awatakase Manani, Mola wetu ni karima
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Nikiwa msikitini,dua naiomba njema
Naonyesha shukrani, kwa malezi yao mema
Kunilea kiimani, mengi yamewasakama
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Mapengo wa visiwani, wewe ni bingwa daima
Nymkomogi Bayani, kuwakilisha Mrima
Mnitoe mashakani, majibu mukiyatuma
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.
Hapa ndiyo kituoni, Mkutubi kadi tama
Nimeshafika mwishoni, hekima ni kusimama
Kalamu naweka chini, nimshukuru Karima
Niwape zawadi gani, wazazi baba na mama.